Mwezi wa kumi huwa ni mwezi maalumu kwa ajili ya kufanya kampeni inayokuza na kueneza uelewa kuhusu afya ya akili (Mental Health Awareness month). Na dhima kubwa ya mwaka huu inasema “Afya ya akili ni haki ya binadamu kwa wote”
Kwa kujua umuhimu wa siku hii na namna gani swala zima la afya ya akili linavyohitaji mjadala mpana nchini Tanzania, Michael na Nadia wameketi chini na kuichambua safari nzima ya afya ya akili hapa nchini Tanzania.
Tunakubaliana na ukweli kwamba kuna hatua zimepigwa kwenye kuhakikisha misaada na ufahamu wa afya ya akili unaongezeka katika jamii, ila lazima tuwe wakweli kwamba bado pengo pia linaonekana.
Mazungumzo ya leo yanatulezea namna ya kugundua changamoto za afya ya akili, umuhimu wa kutafuta msaada, msaada unapopatikana lakini pia, kama hauwezi kumudu gharama za wataalamu, ni nini ambacho unaweza kiufanya mwenyewe ili uweze kujiokoa?
Mazungumzo yote ya leo yamefanyika yakiwa na lengo moja tu, kukufanya uanze kujali afya yako ya akili. Na ndiyo maana kipindi cha leo kinaitwa “Jali afya yako ya akili”